Afisa mmoja mkuu na idara ya watoto ya umoja mataifa UNICEF, anasema takriban watoto elfu 5 wanatumiwa kama wanajeshi huko Somalia, pale Al shabab inapoendelea na kampeni zake za uandikishaji.
Katika mahojiano na idhaa ya kisomali ya sauti ya Amerika, Susannah Price, afisa mkuu wa mawasiliano wa UNICEF, alisema uandikishaji na utumiaji wa watoto kama wanajeshi umeorodheshwa na idadi yake inashtusha.
Anasema hali ni mbaya sana, takriban hadi watoto elfu 5 ni wanajeshi. Anasema tunajuwa kwamba Al Shabab ina kampeni ya kuandikisha watoto, mara nyengine kwa kutumia vishawishi huku wakiwapatia pesa au chakula. Watoto waliopo katika kambi za waliopoteza makazi wanalengwa zaidi na Al shabab.
Hapo siku za nyuma, inakadiriwa watoto elfu 2 hadi 3, wakiwa na umri mdogo wa hata miaka 9, waliandikishwa katika vikosi vya kijeshi vya Somali, hayo ni kwa mujib wa UNICEF.
Bi Price ametaka viongozi wa Somalia kutoa kipaumbele kwa ulinzi wa haki za watoto na kubuni mazingira salama kwa watoto wa Somalia